Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Mhe.Ibrahim Ngwada amefanya kikao na viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini leo siku ya ijuma tarehe 6/7/2022 katika ukumbi wa mikutano wa Manispaa ya Iringa, lengo la kikao hicho ikiwa ni kujadili mustakabali wa masuala ya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto na wanawake.
Akifungua kikao hicho Mhe. Ngwada amefurahishwa na muitikio mkubwa wa viongozi hao na kusema kuwa lengo la kikao hicho ni kujadili jinsi ya kutatua na kukabiliana na na changamoto kubwa ya mmomonyoko wa maadili hususani ulawiti na ubakaji uliokithiri dhidi ya watoto na wanawake katika Manispaa ya Iringa.
Aidha Mhe.Ngwada amesema kumekuwa na ongezeko kubwa sana la kesi za ulawiti ambazo zimekuwa zikiripotiwa polisi Dawati la Jinsia jambo ambalo limepelekea kuwaomba viongozi hao wa dini kulichukua jambo hili ili waweze kuona namna bora ya kupambana na hali hii iliyopo kwa sasa ikiwa ni kwa kutoa elimu zaidi ya kiroho kwa kuwaasa waumini kuacha kabisa matendo hayo maovu ambayo hayampendezi Mwenyezi Mungu pamoja na wanadamu.
Afisa ustawi wa jamii Bi. Tinieli Mbanga ameeleza kuwa walianza kutekeleza afua za ulinzi kwa watoto mwaka wa fedha 2017 – 2018 na ametaja kuwa jumla ya matukio 4651 yameripotiwa ambayo yalihusisha vitendo vya ubakaji, ulawiti kwa watoto, wanawake na vijana kwa ujumla.
Mbaga amesema kuwa njia wanazo zitumia kukabiliana na suala hilo ni kutoa elimu kwa jamii, kuanzisha kamati ya ulinzi na usalama kwa watoto, mpango wa marekebisho wa tabia, makongamano na mikutano ya hadhara
Bw.Justus Basike Mkaguzi Msaidizi wa polisi amesema kuwa wamekuwa wakishughulikia kisheria vitendo vya ukatili ikiwemo ubakaji na ulawiti, na kuwa changamoto wanazo kumbana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao ni ucheleweshwaji wa taarifa na wanafanilia kushindwa kufika mahakamani kutoa ushahidi na kumaliza kesi majumbani.
Aidha ameeleza mbinu wanazo zitumia kukuabiliana na ukatili ikiwemo kutoa elimu ,kushirikiana na ofisi ya ustawi wa jamii ya Manispaa na kufanya doria kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo vilabu vya pombe.
Katika kikao hicho viongozi hao wa dini kwa pamoja wameshukuru uongozi wa Manispaa kwa kuona umuhimu wao na kuwaita kujadiliana kwao ni jambo la faraja, na wameliomba Jeshi la polisi kufatilia kwa karibu vibanda umiza ambavyo vimekuwa ni kichocheo kikubwa cha matukio hayo ya ukatili na kuweka sheria ambazo zitaweza kuwalinda watoto dhidi ya ukatili wa kijinsia.
Mstahiki Meya Mhe.Ngwada amewashukuru viongozi Kwa kuitikia wito huo huku wakiunda kamati ya kupambana na ukatili na ulawiti na kuweka maazimio ishirini na mbili( 22) ambayo yatasaidia kupunguza na kutokomeza kabisa vitendo vya ukatili katika Manispaa hii.
Iringa Municipal Council
Sanduku la Posta: 162
Telephone: +255-2702647
Mobile: 255-2702647
Email: md@iringamc.go.tz
hakimiliki@2017Iringa Manispaa haki zote zimehifadhiwa